Wednesday, 23 May 2012

KURUNZI YA KANISA FM 6


KURUNZI YA KANISA FM
Mengi ninayo kutoka gatuzi la Yerusalemu na vilevile kutoka kitabu cha Matendo ya Mitume. Lakini kwanza tuvipate vimulimuli.
-          Ufisadi waua mja na bibiye...
-          Hotuba ya Paulo...
-          Na nitakueleza ni nani aliyeachiliwa na ni nani aliyeshikwa na mahakama ya  kimataifa.
Hujambo na karibu kwa Kurunzi mimi ni Paul King’ori.
KURUNZI TIMILIFU
Nchi nyingi zimekuwa zikibwatika kwa sababu ya ufisadi. Habari za kusikitisha ni kwamba ufisadi ulipenya hadi kanisani kwa mja mmoja huko Yerusalemu. Mwanaume huyo anayejulikana kama Anania aliuza kipande cha shamba lake lakini akamua kuficha baadhi ya thamani ya mauzo. Kulingana na vile tulivyoarifiwa, Anania alipeleka fedha kwa kamati iliyokuwa ikishughulikia thamani zilizokuwa zikitolewa pale kanisani. Alipoulizwa kama hiyo ndiyo ilikuwa thamani yote alijibu ndiyo. Alikuwa amemghilibu Roho Mtakatifu. Alianguka na kukata roho papo hapo.
  Mwandishi wetu alipata habari kuwa  baada ya saa tatu mkewe yaani Safira alitia habta ya kanisani. Alipoulizwa na mwenyekiti wa kamati, Petero, alijibu kama mumewe. Ghafula bin vuu akaanguka na kufariki. Hayo yakawa malipo ya ufisadi. Chambilecho ya Biblia malipo ya dhambi ni kifo.
  Mwezi wa sita ndio  Dr. Martin Luther King Junior  alitoa hotuba maarufu ya kutotumia fujo katika chuo kikuu cha California. Kwingineko, Mtume Paulo ametoa hotuba maruufu ya maisha katika Kristo. Katika waraka aliouandikia Waefeso nambari ya usajili 4:26, anawashauri na kuwashawishi watende wema. Kinaya ni kuwa anawambia wawe na hasira, ila wasitende dhambi, jua lisichue kama bado na uchungu wao bado hujawatoka. Mwizi asiibe tena bali atende kazi nzuri kwa mikono yake mwenyewe. Halikadhalika, neno lililo ovu lisitoke vinywani mwao bali njema la kumfaa msikilizaji. Toeni maneno ya kuleta neema kwa wasikilizaji wenu. Wasiwe na uchungu, kelele au matukano. Yote ni tisa, la kumi, alisema wawe na huruma na wasahemeane kama Mungu alivyowasamehe  wao katika Kristo.  
   Hivi karibuni Kenya kulifanyika uteuzi wa viongozi wa idara ya mahakama. Kwingineko Yerusalemu, kumefanyika uteuzi wa aina yake. Stefano, Filipo,Prokoro, Nikanoni, Timoni, Paremena na Nikolau waliteuliwa ili kuunda jopokazi la kugawa fedha za msaada. Fedha hizi zilikuwa za kila siku kwa wajane. Haya yalitokea baada ya manung’uniko kuzuka kuwa wajane wa Kiebrania walikuwa wakisahaulika na wale wa Kiyunanikupewa fedha. Jopokazi hili lilipendeza machoni mwa kila mtu na neno la Mungu likaenea kama moto wa nyasi jangwani.

  KURUNZI KIMATAIFA
Maajabu hayataisha duniani. hapo jana binadamu walimpeleka Mwokozi wao, Yesu katika mahakama ya kimataifa. Walimkahifu kwa kudai kuwa yeye ni mwans\a wa Mungu. Ole wao! Jaji mkuu Pilato alimsomea Yesu mshtaka naye hakukana. Huko nje halaiki iliyokuwa imekusanyika huku ikipiga makelele, iliitisha Baraba baada ya Pilato kusema kuwa hamna ushahidi wa kutosha kumhukumu Yesu.
 Jaji hakuwa na lakufanya ila kunawa mikono, ishara kuwa damu ya Yesu haikuwa mikononi mwake. Tanzia ilikuwa kusulubiwa kwa Yesu. Faraja ikawa kufufuka baada ya siku tatu. Bwana apewe sifa. Mathayo 27.
KURUNZI MICHEZONI
Hapo jana mchezaji mashuhuri wa Tenisi Daudi alinyakua ushindi dhidi ya Mfilisti. Daudi aliyemshinda Goliathi kwa pointi 70-02, alijishindia taji la mchezaji bora duniani. Daudi sasa ameshikilia rekodi ya mchezaji mchanga mno kumshinda bingwa mtetezi wa Wafilisti. Daudi alipata ushindi huo baada ya kumuua Goliathi aliyekuwa akiwabeza wana wa Israeli kila uchao. Kutoka Kanisa FM, twampongeza Daudi na sifa zimwendee Mungu wa Isaka na Yakobo.
Kufikia hapo sina la ziada lakini endelea kutegea papa hapa kwa mengine mengi. Kwaheri na hadi wakati mwingine, mimi ni Paul King’ori.


1 comment:

  1. kazi njema kaka.. spoti zimenifurahisha zaidi.. endelea na mtindo uo huo

    ReplyDelete