Wednesday 23 May 2012

KURUNZI YA KANISA FM 6


KURUNZI YA KANISA FM
Mengi ninayo kutoka gatuzi la Yerusalemu na vilevile kutoka kitabu cha Matendo ya Mitume. Lakini kwanza tuvipate vimulimuli.
-          Ufisadi waua mja na bibiye...
-          Hotuba ya Paulo...
-          Na nitakueleza ni nani aliyeachiliwa na ni nani aliyeshikwa na mahakama ya  kimataifa.
Hujambo na karibu kwa Kurunzi mimi ni Paul King’ori.
KURUNZI TIMILIFU
Nchi nyingi zimekuwa zikibwatika kwa sababu ya ufisadi. Habari za kusikitisha ni kwamba ufisadi ulipenya hadi kanisani kwa mja mmoja huko Yerusalemu. Mwanaume huyo anayejulikana kama Anania aliuza kipande cha shamba lake lakini akamua kuficha baadhi ya thamani ya mauzo. Kulingana na vile tulivyoarifiwa, Anania alipeleka fedha kwa kamati iliyokuwa ikishughulikia thamani zilizokuwa zikitolewa pale kanisani. Alipoulizwa kama hiyo ndiyo ilikuwa thamani yote alijibu ndiyo. Alikuwa amemghilibu Roho Mtakatifu. Alianguka na kukata roho papo hapo.
  Mwandishi wetu alipata habari kuwa  baada ya saa tatu mkewe yaani Safira alitia habta ya kanisani. Alipoulizwa na mwenyekiti wa kamati, Petero, alijibu kama mumewe. Ghafula bin vuu akaanguka na kufariki. Hayo yakawa malipo ya ufisadi. Chambilecho ya Biblia malipo ya dhambi ni kifo.
  Mwezi wa sita ndio  Dr. Martin Luther King Junior  alitoa hotuba maarufu ya kutotumia fujo katika chuo kikuu cha California. Kwingineko, Mtume Paulo ametoa hotuba maruufu ya maisha katika Kristo. Katika waraka aliouandikia Waefeso nambari ya usajili 4:26, anawashauri na kuwashawishi watende wema. Kinaya ni kuwa anawambia wawe na hasira, ila wasitende dhambi, jua lisichue kama bado na uchungu wao bado hujawatoka. Mwizi asiibe tena bali atende kazi nzuri kwa mikono yake mwenyewe. Halikadhalika, neno lililo ovu lisitoke vinywani mwao bali njema la kumfaa msikilizaji. Toeni maneno ya kuleta neema kwa wasikilizaji wenu. Wasiwe na uchungu, kelele au matukano. Yote ni tisa, la kumi, alisema wawe na huruma na wasahemeane kama Mungu alivyowasamehe  wao katika Kristo.  
   Hivi karibuni Kenya kulifanyika uteuzi wa viongozi wa idara ya mahakama. Kwingineko Yerusalemu, kumefanyika uteuzi wa aina yake. Stefano, Filipo,Prokoro, Nikanoni, Timoni, Paremena na Nikolau waliteuliwa ili kuunda jopokazi la kugawa fedha za msaada. Fedha hizi zilikuwa za kila siku kwa wajane. Haya yalitokea baada ya manung’uniko kuzuka kuwa wajane wa Kiebrania walikuwa wakisahaulika na wale wa Kiyunanikupewa fedha. Jopokazi hili lilipendeza machoni mwa kila mtu na neno la Mungu likaenea kama moto wa nyasi jangwani.

  KURUNZI KIMATAIFA
Maajabu hayataisha duniani. hapo jana binadamu walimpeleka Mwokozi wao, Yesu katika mahakama ya kimataifa. Walimkahifu kwa kudai kuwa yeye ni mwans\a wa Mungu. Ole wao! Jaji mkuu Pilato alimsomea Yesu mshtaka naye hakukana. Huko nje halaiki iliyokuwa imekusanyika huku ikipiga makelele, iliitisha Baraba baada ya Pilato kusema kuwa hamna ushahidi wa kutosha kumhukumu Yesu.
 Jaji hakuwa na lakufanya ila kunawa mikono, ishara kuwa damu ya Yesu haikuwa mikononi mwake. Tanzia ilikuwa kusulubiwa kwa Yesu. Faraja ikawa kufufuka baada ya siku tatu. Bwana apewe sifa. Mathayo 27.
KURUNZI MICHEZONI
Hapo jana mchezaji mashuhuri wa Tenisi Daudi alinyakua ushindi dhidi ya Mfilisti. Daudi aliyemshinda Goliathi kwa pointi 70-02, alijishindia taji la mchezaji bora duniani. Daudi sasa ameshikilia rekodi ya mchezaji mchanga mno kumshinda bingwa mtetezi wa Wafilisti. Daudi alipata ushindi huo baada ya kumuua Goliathi aliyekuwa akiwabeza wana wa Israeli kila uchao. Kutoka Kanisa FM, twampongeza Daudi na sifa zimwendee Mungu wa Isaka na Yakobo.
Kufikia hapo sina la ziada lakini endelea kutegea papa hapa kwa mengine mengi. Kwaheri na hadi wakati mwingine, mimi ni Paul King’ori.


Friday 4 May 2012

KURUNZI YA KANISA FM 5

KURUNZI YA KANISA FM
Wakati umenipa kibali ili niweze kukuletea habari jamali. Asanti sana kwa kujiunga nami nikikumulikia yaliyojiri kwa ijili. Lakini kwanza kawaida yetu ni kuvipata vimulimuli. 

VIMULIMULI
- Kinyesi kikavu chapika...
- Tutaangalia vita dhidi ya wanamgambo wa kiroho...
- na Michezoni Nehemia ashinda Tobia.
Hujambo na karibu mimi ni msimulizi wako Paul King’ori.

KURUNZI TIMILIFU

TAHADHARI: Mwelekezi wangu ananiarifu kuwa habari ifuatayo yaweza kuzua hisia zisizoridhisha hususan kama watafuna. Hata hivyo, ni ukweli mtupu... Nabii Ezekieli alipitia mateso ya aina yake huko Yerusalemu. Licha ya kuagizwa alalie kaure kwa siku 390, alikuwa anafungwa kwa kamba na Mungu ili asipinduke. Hii ni ishara ya vile Israeli watakavyofungwa utumwani. Hicho kilikuwa ni kionjo cha kiroja. Kilele chake kilikuwa cha kushangaza zaidi. Uhalisia ni kuwa kinyesi hutumika kuzalisha kawi. Aghalabu kawi yenyewe hutumika kupikia. Hata hivyo, mwenyezi Mungu alimweleza  Ezekieli apike kwa kinyesi cha binadamu. Ndiyo, cha binadamu. Mungu alimwamuru nabii huyo aoke mkate kutumia kinyesi kikavu. Haya yanaashiria uchafu wa dhambi za Yerusalemu. Ezekieli alipewa maelezo hayo na alipomlalamikia Mungu ya kuwa hajajichafua, Mungu alimhurumia na akamwambia aoke mkate wake kwa kinyesi cha ng’ombe kama mbadala. Hii ikawa ni ishara ya vile watakavyokula chakula kichafu kwa kuzidiwa na dhambi.
 Hayakuishia hapo. Aliambiwa anyoe ndevu na kichwa chake, kisha aigawe nywele aliyokata katika matuta. Alikuwa achome thuluthi moja, thuluthi nyingine aikate kwa upanga na nyingine aitawanye kwa upepo. Ya Mungu ni mengi na hiyo ni gharama ya dhambi dhidi yake. Ripoti hii ni kutoka Ezekieli 4 na 5.
Nyakati hizi za kisasa, nchi nyingi zimeshuhudia uhaba wa chakula. Hata hivyo gatuzi la Galilaya lilipata chakula cha msaada kutoka mbinguni (ama ukipenda Heaven For Galilee). Haya yalifuatia baada ya siku tatu za makali ya njaa. Makamu wa Rais aliwaonea huruma na kufanyia mikate mitano na samaki wawili mujiza. Bidhaa hizo zilikuwa chakula kingi mno cha thamani ya mamilioni ya pesa. Chakula hicho kiliishibisha halaikiya watu elfu tano! Kwa mujibu wa mmoja wa waliokula, aliyejitambulisha kama Mariko, alisema kilikuwa kitamu kupindukia na hata walibakisha vikapu kumi na viwili.
 Kinaya ni kuwa mujiza huu haukulipishwa kama miujiza mingi ya siku hizi. Kwa habari zaidi, tumia anwani ya mtandao ifuatayo. Holybible@ mark6.36-41.com

KURUNZI BIASHARA
  Huku shilingi ya Kenya ikiendelea kupoteza thamani kwa kasi, nchi ya Yerusaremu hivi karibuni huenda ikaanza kulia kivulini. Walakini lazima wananchi wafuate masharti ya Mwenyezi Mungu. Inawalazimu kutupilia mbali dhambi zao. Kulingana na kituo cha habari cha Isaya 55.1, Wanayerusaremu wataanza kula mikate na kunywa divai na maziwa bila kulipa hata thumni! Haya yatawezeshwa na Mungu mwenyewe ili wajue kuwa yeye ndiye Mungu Muumba na  kwamba yuamiliki kila kitu duniani. Wito wa usaidizi huo umepeanwa na Mola kupitia kwa msemaji wake nabii Isaya, huku akisema kuwa nia zenu si kama zake  wala mawazo yake kama yenu.

KURUNZI KIMATAIFA
   Hivi karibuni tumeshuhudia vita baina ya jeshi la Kenya na wanamgambo wa Al-Shabaab. Aghalabu vita hufanyika baina ya watu au nchi. Hii ni dhihirisho tosha kuwa vita ni vya aina nyingi. Uhalisia ni kuwa sisi Wakristo hatupigani vita vya kimwili ila twapigana vya Kiroho dhidi ya mwovu na ujanja wake. Hivyo basi ni muhimu kutumia silaha za kiroho, ili tushinde hivi vita. Baadhi ya silaha hizi ni; Mshipi wa Ukweli, kifuani tuvalie Utakatifu, viatu vya Ubashirina, ngao ya Imani, helmeti ya Wokovu na sime ya Neno la Mungu. Aidha tutumie gari la Maombi. Usaidizi wa Mungu utakaotokana na maombi ndio utakaokuwa mafuta ya magari yenu. Hii ni ripoti kutoka waraka wa Paulo kwa Waefeso 6:10-18.

KURUNZI MICHEZONI
   Katika michezo, timu ya Nehemia iliihemesha timu ya Tobia na Sanbalati huko Yerusalemu. Timu ya Sanbalati ilikuwa imekula njama ya kumchezea Nehemia vibaya,  kumjeruhi uwanjani na hatimaye kumuua. Ilifumbuliwa kuwa Sanbalati walikuwa wamepanga kumtega Nehemia uwanjani wa kujengea Ukuta. Hata hivyo Nehemia aliikwepa mikiki ya Tobia na kukataa kula mtama aliomwagiwa na akaendelea na kazi ya ujenzi wa ukuta. Hapo ndipo alipowafungia mabao saba kwa nunge kwani hawakumpata wamdhuru. Ripoti hiyo ya Nehemia 6 ndiyo inatukamilishia Kurunzi kwa sasa. Asanti kwa kunipa makini yako. Mungu akubariki na ukumbuke kumwombea mwenzako. Hadi wakati mwingine, mimi ni Paul King’ori.