KURUNZI
YA KANISA FM
Mengi ninayo kutoka
gatuzi la Yerusalemu na vilevile kutoka kitabu cha Matendo ya Mitume. Lakini
kwanza tuvipate vimulimuli.
-
Ufisadi waua mja na bibiye...
-
Hotuba ya Paulo...
-
Na nitakueleza ni nani aliyeachiliwa na
ni nani aliyeshikwa na mahakama ya
kimataifa.
Hujambo na karibu kwa Kurunzi mimi ni Paul King’ori.
KURUNZI
TIMILIFU
Nchi nyingi zimekuwa zikibwatika
kwa sababu ya ufisadi. Habari za kusikitisha ni kwamba ufisadi ulipenya hadi
kanisani kwa mja mmoja huko Yerusalemu. Mwanaume huyo anayejulikana kama Anania
aliuza kipande cha shamba lake lakini akamua kuficha baadhi ya thamani ya mauzo.
Kulingana na vile tulivyoarifiwa, Anania alipeleka fedha kwa kamati iliyokuwa
ikishughulikia thamani zilizokuwa zikitolewa pale kanisani. Alipoulizwa kama
hiyo ndiyo ilikuwa thamani yote alijibu ndiyo. Alikuwa amemghilibu Roho
Mtakatifu. Alianguka na kukata roho papo hapo.
Mwandishi wetu alipata habari kuwa baada ya saa tatu mkewe yaani Safira alitia
habta ya kanisani. Alipoulizwa na mwenyekiti wa kamati, Petero, alijibu kama
mumewe. Ghafula bin vuu akaanguka na kufariki. Hayo yakawa malipo ya ufisadi. Chambilecho
ya Biblia malipo ya dhambi ni kifo.
Mwezi wa sita ndio Dr. Martin Luther King Junior alitoa hotuba maarufu ya kutotumia fujo katika
chuo kikuu cha California. Kwingineko, Mtume Paulo ametoa hotuba maruufu ya
maisha katika Kristo. Katika waraka aliouandikia Waefeso nambari ya usajili 4:26,
anawashauri na kuwashawishi watende wema. Kinaya ni kuwa anawambia wawe na
hasira, ila wasitende dhambi, jua lisichue kama bado na uchungu wao bado
hujawatoka. Mwizi asiibe tena bali atende kazi nzuri kwa mikono yake mwenyewe. Halikadhalika,
neno lililo ovu lisitoke vinywani mwao bali njema la kumfaa msikilizaji. Toeni maneno
ya kuleta neema kwa wasikilizaji wenu. Wasiwe na uchungu, kelele au matukano. Yote
ni tisa, la kumi, alisema wawe na huruma na wasahemeane kama Mungu
alivyowasamehe wao katika Kristo.
Hivi karibuni Kenya kulifanyika uteuzi wa
viongozi wa idara ya mahakama. Kwingineko Yerusalemu, kumefanyika uteuzi wa
aina yake. Stefano, Filipo,Prokoro, Nikanoni, Timoni, Paremena na Nikolau
waliteuliwa ili kuunda jopokazi la kugawa fedha za msaada. Fedha hizi zilikuwa
za kila siku kwa wajane. Haya yalitokea baada ya manung’uniko kuzuka kuwa
wajane wa Kiebrania walikuwa wakisahaulika na wale wa Kiyunanikupewa fedha. Jopokazi
hili lilipendeza machoni mwa kila mtu na neno la Mungu likaenea kama moto wa
nyasi jangwani.
KURUNZI KIMATAIFA
Maajabu hayataisha duniani.
hapo jana binadamu walimpeleka Mwokozi wao, Yesu katika mahakama ya kimataifa. Walimkahifu
kwa kudai kuwa yeye ni mwans\a wa Mungu. Ole wao! Jaji mkuu Pilato alimsomea
Yesu mshtaka naye hakukana. Huko nje halaiki iliyokuwa imekusanyika huku
ikipiga makelele, iliitisha Baraba baada ya Pilato kusema kuwa hamna ushahidi
wa kutosha kumhukumu Yesu.
Jaji hakuwa na lakufanya ila kunawa mikono,
ishara kuwa damu ya Yesu haikuwa mikononi mwake. Tanzia ilikuwa kusulubiwa kwa
Yesu. Faraja ikawa kufufuka baada ya siku tatu. Bwana apewe sifa. Mathayo 27.
KURUNZI
MICHEZONI
Hapo jana mchezaji mashuhuri
wa Tenisi Daudi alinyakua ushindi dhidi ya Mfilisti. Daudi aliyemshinda
Goliathi kwa pointi 70-02, alijishindia taji la mchezaji bora duniani. Daudi sasa
ameshikilia rekodi ya mchezaji mchanga mno kumshinda bingwa mtetezi wa
Wafilisti. Daudi alipata ushindi huo baada ya kumuua Goliathi aliyekuwa
akiwabeza wana wa Israeli kila uchao. Kutoka Kanisa FM, twampongeza Daudi na
sifa zimwendee Mungu wa Isaka na Yakobo.
Kufikia hapo sina la
ziada lakini endelea kutegea papa hapa kwa mengine mengi. Kwaheri na hadi
wakati mwingine, mimi ni Paul King’ori.