Saturday 10 March 2012

KURUNZI YA COMMISSION

KURUNZI YA KANISA FM
“ Huu ndio wito, kuwa mashahidi wa Kristo.
Tu wafanyikazi waaminifu. Tumejazwa nguvu na upendo.
Tumetumwa kote duniani.
Yesu nisaidie, Bwana nisaidie, kwa kuwa huu ndio wito.”
  Hiki ni kibwagizo cha wimbo wa maudhui ya Commision 2011. Wimbo wenyewe uliandikwa na Terry Nzaumi, kutoka Kenya Methodist University.
Mengi ninayo lakini kwanza tupate vimulimuli vya Kurunzi. 

VIMULIMULI
... Maelfu yakusanyika katika kongamano…
… Rais Mstaafu awashangaza wengi kwa kunukuu Biblia…
… Tamasha la mwaka mpya lawasha moto…
… na Wanamoi wajaa Kabarak.
Hujambo na karibu nikutaarifu kikamilifu. Mimi ni Paul King'ori.

KURUNZI TIMILIFU
   Jumatano ya tarehe 28 Disemba mwaka jana ilikuwa ni siku ya wajumbe kusafiri. Barabara zote, za Kenya na Afrika Mashariki zilielekea mji mtulivu na safi wa Nakuru, Chuo kikuu cha Kabarak. Chuo chenyewe kina mandhari ya kuvutia,tulivu na ina mijengo ya kisasa. Kwa mujibu wa habari tulizokusanya dakika chache baada ya kuwasili, zilisema kuwa wajumbe walianza kuingia Kabarak saa mbili asubuhi. Wajumbe walikuwa wametoka; Kenya, Uganda, Tanzania, Rwanda, Ethiopia, Sudan ya Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Malawi, Nigeria na Norway.
   Idadi iliyokuwako ni takribani elfu tatu mia tano. Usajili wa idadi hiyo kubwa ya wajumbe ulileta matatizo ya hapa na pale. Ilibidi usitishwe ili wajumbe wapate chajio na wamshukuru Mungu kwa safari njema. Usajili uliendelea hadi saa sita usiku, siku hiyo ya kwanza. Mathalan, kawaida ni kama sheria. Kuna wajumbe walikuwa wanaingia saa tatu za usiku.
   Siku ya pili, Rais mstaafu Daniel Toroitich arap Moi aliwasili, aliwakaribisha wajumbe na kufungua kongamano rasmi. Usisahau kuwa ndiye mdhamini mkuu wa chuo hicho. Usiudharau wembamba wa reli, gari la moshi hupita, alikuwa akinukuu vifungu vya Biblia na kuwaacha wajumbe wengine vinywa wazi.
   Baada ya idhini kutoka kwa mwenye nyumba, kongamano lilianza mara moja, huku Askofu David Oginde akizichambua changamoto za kusikiza. Umuhimu wa somo hili  kuanza ulikuwa kuwafungua wajumbe ili waweze kusikiza mengine yote yaliyofuatia.
   Kongamano lenyewe, lilikuwa la nane lililoandaliwa na Ushirika wa Miungano ya Wakristo wa Kenya, ukipenda, “FOCUS Kenya”. Kaulimbiu ya kongamano ilikuwa ni kutoka Yohana 20:21 isemayo, “Kama baba alivyonituma, nami nawapeleka ninyi.” Kisisitizi kikiwa “Tumeitwa tuwe mashahidi waaminifu.” Masomo yote yalizunguka kaulimbiu. Kwa hivyo tulifunzwa mengi kuhusu ubashirina au misheni.

~~~CHEUO~~~

   Wazungumzaji katika kongamano walikuwa ni Femi Adeleye kutoka Nigeria, Steve Maina aliye na huduma New Zealand, Dkt. Antonia Leonara van der Meer, kutoka Brazil,aliyekuwa mwanafunzi wa Chuo kikuu cha Moi, Peter Oyugi anayehudumu London, Uingereza,Mchungaji Calisto Odede wa NPC Karen, Mchungaji Francis Omondi kutoka Kenya, Dkt. Timothy Wachira, mhadhiri mkuu wa Chuo Kikuu cha Daystar, Dkt, Stanley Mukolwe kutoka Kenya, Profesa Mark Shaw kutoka Kenya, Mchungaji Elisha Onditi Odero kutoka Kenya na Eric Simiyu wa kipindi cha Hope FM cha “Yesu Ndiye Njia”.
   Kila siku ilianza kwa nyimbo za sifa na za kuabudu, kisha ukariri wa sura mbalimbali lakini mtawalia za Danieli. Ukariri ulifutwa na uchambuzi wa kitabu cha Danieli naye Mchungaji Femi Adeleye. Baada ya kusoma Biblia katika vikundi, wajumbe walitawanyika na kuingia katika vyumba tofauti ili wahudhurie warsha tofauti zilizogusia nyanja mbalimbali za maisha ya binadamu na huduma ya Injili, kwa mfano; kutafuta kazi, ufanisi masomoni, dhima ya nyimbo katika huduma, mapenzi na uhusiano,haki za kikatiba, vyombo vya habari katika huduma, urembo na mapambo, utandawazi, siasa za wanafunzi,kwa kutaja machache tu.
   Chamcha ilifuatwa na wakati wa utangamano baina ya watu na wenzao au kati yao na taasisi tofauti zilizokuwa zina maonyesho. Baada ya utangamano, wajumbe walihudhuria warsha zingine. Saa kumi unusu walirudi katika hema na kuendelea na kongamano hadi saa kumi na mbili, walipotawanyika kwa chajio. Awamu ya nne ya kongamano ilianza saa moja unusu kwa ibada na michezo ya kuigiza na kuisha saa tatu unusu.
   Mkesha wa mwaka mpya kulikuwa na tamasha la kusisimua si haba. Wajumbe kutoka karibu na mbali waliwasilisha vipawa tofauti vilivyolenga tamaduni zao. Kulikuwa na nyimbo, mavazi ya kitamaduni na mashairi.
 Wajumbe wote walishirikiana kuhesabu sekunde chache kabla ya mwaka kuruka. Uliporuka, shangwe,nderemo,mbinja na nyimbo zilitanda kote. Ungedhani ni ujenzi wa babeli. Baada ya moto wa kuruka mwaka kufifia, maombi ya mwaka yalifanywa. Hata hivyo sherehe ziliendelea baada ya maombi. Watu wana nguvu, walijitingisha na kushangalia nje ya hema hadi usiku wa manane.
CHAKULA
   Vyakula vya kiroho na vya kimwili vilikuweko kwa wingi, hata hivyo,ili mjumbe ale, lazima angemiliki kadi ya mlo, maarufu kama meal card. Sadfa ni kuwa, tulisoma Danieli 1:15 na kuona kuwa Danieli walipewa mboga na afya yao ikanawiri. Amini usiamini, hamna mlo uliokosa kabeji na sukuma wiki! Hata hivyo, Kurunzi iligundua kuwa nyama za aina tofauti zililiwa kila siku. Kinaya ni kuwa kina dada walitufeli kwani walikuwa wanashindwa kumaliza chanjo nne za mkate wa kiamsha kinywa. Nne peke yake! Chakula kilikuwa kingi hadi watu wengine wakaripotiwa kuongeza uzani.
   Chakula cha kiroho kilikuwa ni nyimbo zilizonyunyizia nyoyo za wajumbe uwepo wa Mungu, na mafunzo ya Bibilia. Kwaya iliyoundwa na wajumbe kutoka nchi tofauti ilikuwa inasifu nusura hema lipasuke. Vitabu vilikuwa vingi kwa bei nafuu, wajumbe walikuwa na ugumu wa kuchagua watakavyovinunua na pia walipewa vingine bila malipo.
   Siku ya mwisho ndiyo iliyokuwa ya kuwapeleka au kuwatuma wajumbe ili waende kubashiri. Hapo uwepo wa Mungu ukadhihirika kama mchana wa jua. Wengine waligaagaa na kutoa sauti za kunyenyekea kwa kupigwa na nguvu za Mungu. Wengine walilia kwa hisia nzito za mapenzi ya kwenda walikotumwa na Bwana na wengine walikaa kupigwa na butwaa. Uhalisia ni kwamba, Injili ina mustakabali mwema uliojaa matumaini. Bwana apewe sifa!
   Wajumbe walikuwa na matarajio mengi na ndoto nyingi zilitimizwa kwa uwezo wa Mungu. Hata hivyo waandalizi walionya hawatachukua jukumu lolote lile abadan katan katika maisha ya wajumbe baada ya kongamano.
   Hatimaye waumini wa chuo kikuu cha Moi walikuwa wengi mno hivi kwamba ungedhani uko katika bewa kuu la Chuo hiki. Kwa waliohudhuria, asanteni kwa kusikia wito, kwa waliokosa Ezra 2012 i njiani, hakikisha umehudhuria. Mungu awabariki.
   Kwa niaba ya wale wote walizipika habari hizi hadi zikaimarika, nakushukuru kwa kunipa makini na masikio yako... Hadi wakati mwingine, kwaheri. Mimi ni Paul King'ori.

No comments:

Post a Comment