Saturday 24 March 2012

SHAIRI LA VIONGOZI

  VIONGOZI-Na Paul King'ori
Mmeipita mipaka, wazalendo waumia,
Wanazidiwa kumaka, huku pia wakilia,
Viongozi ninafoka, leo nawashambulia.
Viongozi ongozeni, kwa imani na mani

Mwadhulumu wazalendo, hamuijui na haki,
Mwawaogoza kwa fundo, ukweli nyi wazandiki,
Bayana hamna pendo, na hili nimehakiki.
Viongozi ongozeni, Kwa imani na amani.

Hongo na mnaitisha, dhahiri hamna soni,
Sikosei mwatadisha, maisha ni benibeni,
Nyinyi mwajifurahisha, wazalendo pasi kani.
Viongozi ongozeni, kwa imani na amani.

Uongozi wenu mwovu, sababu mwafuja mali,
Mwasema muwepevu, hamwishi kwa udhalili,
Mtanyakiwa kwa wavu, ufisadi ni majili.
Viongozi ongozeni, kwa imani na amani.

Mwatembelea waganga, ili mpate nyadhifa,
Nakuli kinaganaga, mwatuletea maafa,
Acheni kuleta janga, isikizeni kaifa.
Viongozi ongozeni, kwa imani na amani.


Kamwe hamna amani, migogoro mnazua,
Mmekuwa wapingani, amanini kutotua,
Mnachochea zogoni, kitali kutotatua,
Viongozi ongozeni, kwa imani na amani.

Leo hi mwanena mama, keshoye mwasema baba,
Mambo yaenda mrama, ukweli kenu ni haba,
Nyi chanzo cha hasama, yakini kosa haiba!
Viongozi ongozeni, kwa imani na amani.

Hitimisho nimefika, kalamu naweka chini,
Si uongo nimeng’aka, ukatili kaburini,
Acheni kuzururuka, gutukeni kwa halani.
Viongozi ongozeni, kwa imani na amani.

No comments:

Post a Comment