Saturday 24 March 2012

KURUNZI YA KANISA FM 4

KURUNZI YA KANISA FM
   “Kama mlivyompokea Kristo kama Bwana, basi nendeleeni kuishi ndani yake.” Hayo ni maneno yaliyosemwa na Paulo katika waraka wake kwa waumini wa Kolosia, S.L.P. Wakolosai 2:6. Kwa upande mwingine, ndiyo maudhui ya siku hii ambayo ni ya kusherehekea panda shuka za maisha ya chuo kikuu na kuwaaga wakongwe wetu. Hayawi hayawi hatimaye huwa. Hauchi hauchi hatimaye hukucha. Ilikucha siku moja wakajiunga na chuo kikuu na imekucha nyingine waondoke. Hawa ni wakongwe wetu. Mengi tunayo ya kuwamulikia lakini kwanza tuvipate vimulimuli.
VIMULIMULI
… Tutaangalia panda shuka za maisha ya wakongwe hapa chuoni…
…Tunazo habari za Oparesheni ya kulinda watakatifu…

... Na Divided Losers wazidiwa na masaibu.
KURUNZI TIMILIFU
  Waliingia chuoni mwaka wa 2007 na 2008. Hiyo ni miaka mitano na minne mtawalia iliyopita. Tunawazungumzia wakongwe tunaowapenda wanaofika hatima ya masomo yao ya hapa. Baadhi yao wakizungumza na Kanisa FM, walinukuu Biblia Zaburi 37:25 isemayo kuwa “Nilikuwa mchanga lakini sasa nimekomaa na sijaona mwaminifu akiwa ameachwa na Mungu.” Walisema kuwa watoto waliopewa wa kiroho hawajawahi omba chakula kwa uaminifu wake Mungu.
   Hata hivyo, walikumbuka kwa wepesi matatizo waliopitia wakiwa chuoni. Waliorodhesha migomo miwili. Mmoja hapo 2008 uliotokana na kupandishwa kwa nauli kupindukia, mgomo wenyewe ulisababisha vifo vya wanafunzi wawili. Wa pili ni mwaka jana uliohusisha shule ya Uhandisi wakati wa mitihani yao. Mitihani hiyo ilicheleweshwa hadi mwanzo wa mwaka huu. Wengine walisema wamekula magunia ya  sukuma mihula yote bila kubadilisha. Tatizo lingine kuu ni lile la kukosa malazi kila mwaka. Hili ni tatizo walilolikuta, na inaonekana ya kuwa wataliacha kama halijapata suluhisho. Ole wenu mnaobakia chuoni!
 Matatizo hayakuishia hapo, ukosefu wa fedha, kazi nyingi za ziada baada ya wahadhiri wakati mwingine kususia mihadhara na kukimbia mwishoni wa muhula na ukosefu wa wakati kwa pilkapilka  za hapa na pale.
 Hata hivyo, sio matatizo pekee waliokumbana nayo. Rika hili liliweza kushuhudia mengi ya kuonewa fahari. Injili iliyonoga katika chuo kikuu cha Moi almaarufu Varsity Mission 2010 pia ni swala la kuangaziwa kwani lilipata ufanisi mkubwa. Hii ni kutokana na ukombozi wa nyoyo na kubadilisha maisha ya watu wengi. Tukio kama hili linatarajiwa hapo mwakani. Halikadhalika, baadhi yao wameshiriki katika ubashirina huko Turkana unaojulikana kama Tri-Annual Mission. Mwisho wa mwaka jana, walihudhuria kwa wingi kongamano la Commision 2011. Hongera nyote mlioshiriki kwa hali na mali.
  Kwingineko waziri wa mashauri na mipango maalumu ya Kiroho Daktari Isaya akihutubia mkutano wa hadhara alinukuliwa akisema kuwa Mungu wetu ni wa maajabu mno. Huku akitoa mfano alisema kuwa Mungu huweza kunena kuhusu tamati ya jambo fulani akiwa ameshika asili yake. Aliongeza kuwa Mungu huhakikisha kuwa neno lolote lake litaishi milele na litatekeleza wajibu wowote ambao limetengewa kufanya. Ujumbe huu umetoka Isaya 46:8-11. Na kwa hivyo wanaomtumainia bwana watabarikiwa adui wapende wasipende.
--CHEUO--
KURUNZI KIMATAIFA
  Ndege ya kivita aina ya Drone imewarushia makombora mazito wafuasi wa kundi haramu la shetani. Hii ni kutokana na juhudi ya Oparesheni ya kulinda watakatifu ambayo imeingia siku yake ya miaka mingi. Majeshi  ya watakatifu wakiongozwa na Amiri jeshi mkuu ambaye ni Yesu Kristo lilichukuwa mwelekekeo mpya baada ya kundi hilo haramu kuoenekana  kufanya uhalifu mara kwa mara dhidi ya walokole. Ibilisi na kundi lake sasa limeachwa bila makao, njaa na kiu hali iliyopelekea wao kuhangaika duniani almaarufu kama World Tarmacking Network, la kufurahisha ni kuwa, hakuna matumaini.
  Kwingineko meli aina ya MV spirit imewateka nyara maharamia wengine wa kundi lilo hilo ambalo kwa sasa wanasubiri kusikizwa kwa kesi yao. Kwa kuwa mahakama ya kimataifa imeonekana haitaweza kuisikiza kesi hiyo, basi bila shaka watafikishwa kwenye mahakama ya Mbinguni. Hii imezua mtafaruku na mahangaiko kati ya wafuasi wengine. Kutokana na hali hii, kituo cha utangazaji cha Kanisa kinaomba kwa dharura injili na maombi kwa kundi hilo ili kuweza kukombolewa.
  Kesi ambayo haikupewa nafasi abadan katan ya kukata rufaa, iliyomkabili aliyekuwa wakati mmoja malaika mkuu aliyeachishwa kazi yake yenye ustaha mkubwa iliamuliwa mara moja. Kwenye uamuzi wake, jaji mkuu mwenye neema kubwa kubwa na ndogo ndogo tena mwenye hekima alimmwagisha unga malaika huyo kwa utovu wa nidhamu ya kutaka kuongezwa madaraka ili kutoshana na bosi wake. Yamkini alitaka kuienzi dunia bila adhari ya kuwa njia panda zilimshinda fisi.
KURUNZI MICHEZONI
  Kwa mujibu wa ripota wetu ambaye ni mwinjilisti Paulo, kinyang’anyiro kati ya malaika huyo ambaye sasa ana jina la kuogofya, ambalo ni shetani, na watakatifu bado inaendelea katika dakika zake za mwisho mwisho almaarufu dakika za ziada. Madhumuni ya kinyang’anyiro hicho ni kujizolea wafuasi wengi. Tahadhari kulingana na ripota wetu ni kuwa mtu yeyote akishawishika kufuata itikadi na mienendo ya ibilisi huyo basi bila shaka atatupwa pamoja na bosi wake katika ziwa la moto. Lakini afueni ni kuwa akiungama na kukiri dhambi zake basi bila shaka atasamehewa na mabaki ya akaunti yake ya M-Dhambi kubakia sufuri bin hamna.
  Hatimaye, mashabiki wengi wanayeunga mkono kwa dhati malaika mtakatifu wameonekana wakiimba nyimbo za kumtukuza na kumuenzi kocha wao ambaye ni Mungu mwenyewe kwa furaha kwani wameamini kwa nyoyo zao kuwa ushindi ni upande wao. Hii imeshuhudiwa katika maeneo mengi humu duniani kama vile katika Muungano wa Wakristo wa Chuo Kikuu Cha Moi, katika ibada ya leo ya kuwaaga wakongwe wao. Kwa upande mwingine, timu ya Divided Losers ikiongozwa na kocha wao, shetani imeonekana ikilemewa kwani kila sekunde, kuna kubadili wachezaji,mahangaiko, kukosa kuelewana, kulaumiana na hata kurushiana makonde mazito mazito, wenyewe kwa wenyewe wakiwa hapa duniani. 
Kwa hayo tunahitimisha Kurunzi lakini jiunge nasi wakati mwingine ili tumulike mengine. 
Nakutakia wakati usio na kero au kerezo. Ni mimi mwandishi wako Paul King'ori.
Imetayarishwa na Theorry Nahashown-(theuristheory@yahoo.com)na Paul King’ori-(wpaulkingori@yahoo.com).




No comments:

Post a Comment