Saturday 24 March 2012

SHAIRI LA HARUSI

UA LANGU
Tumba langu tumba langu, lakunena ndilo sina.
Furaha yangu ja wingu, rohongu zidi kunona.
Meamua hiki chungu, kiwe shamba we hazina
Wanukia wavutia, ua langu umrembo.

Ulipokuwa wakua,  wengi litamani kwona.
Bawabu liweka ua,  dhuluma sije kwona.
Kaweka maji mbolea,  kivuli pasi kuguna.
Wanukia wavutia,  ua langu umrembo.

Umekua kwa madaha, wayafuata madili.
Leo mi nina furaha, eti twaenda manzili.
Nyumbetu iwe na raha, tusigawe mara mbili.
Wanukia wavutia, ua langu umrembo.

Harufuyo yanukia, kila nyuki yavutia.
Takulinda ja malkia, hakuna takufikia,
Penzi mia fil mia, hakiki hutaumia.
Wanukia wavutia, ua langu umrembo.

Umbo lako ni kiungo, rangi nayo yavutia.
Penzi lako kama tango, roho yangu yatulia.
Kikwona kwa mlango, macho siwezi zibia.
Wanukia wavutia, ua langu umrembo.

Nywele nayo maridadi, inang’ara kama mwezi.
Mwangaza pia wazidi, kwa macho ya chipukizi.
 Sauti yako waridi, yapendeza msikizi
Wanukia wavutia, ua langu umrembo.


Siku ya leo nakwoa, mahaba takupa tele.
Hakikisho hujanoa, hiyo pete kwa kidole.
Ndoa yetu naombea, twishi pamoja milele.
Wanukia wavutia, ua langu umrembo.

Nashukuru wakulima, kwa kutunza hili ua.
Ua mesimama wima, sababu ya kununua.
Ua hili ni lizima, pongezi kwa wakulima.
Wanukia wavutia, ua langu umrembo.

Na ya tisa ndiyo beti, kushukuru hi hadhira.
 Metulia kwenye viti, tazama pasi hasira.
Kishuhudia masharti, ya penzi hili duara.
Wanukia wavutia, ua langu umrembo.

Beti kumi nafikia, ua langu kisifia.
Si eti memalizia, wakati ndo wafifia.
Kuondoka naumia, kidosho kutomwimbia.
Wanukia wavutia, ua langu umrembo.


                                                                                       © PAUL KING’ORI,2009

No comments:

Post a Comment