Saturday 24 March 2012

SHAIRI LA UKIMWI

UKIMWI
Machozi yatudondoka, kwa hofu ya tulojua.
Hapa nami nagutuka, laiti wangelijua.
Mapenzi tulojitwika, kwao ja mchana jua.
Ukimwi hauna dawa, tiba wala kafaara.

Madawa twayanunua, nasi tunafilisika.
Hatuna kwa kufunua, mwelewa twasikitika.
Twajaribu kupanua, nasi tu twatilifika.
Ukimwi hauna dawa, tiba wala kafaara.

Watuacha bila mali, watoweka no wazazi.
Chakula hata hatuli, twatorokwa na pumzi.
Hatuwezi kaa tuli, na hatupati ng’o ndizi.
Ukimwi hauna dawa, tiba wala kafaara.

Maisha waliyapenda, si mengine tu anasa.
Walipenda lipya tunda, hata hilo kutomasa.
Wafurahia kutenda,vitendo vyaleta tasa.
Ukimwi hauna dawa, tiba wala kafaara.

Ole wao! Wenye neno,eti ukimwi ni homa.
Waungana yo mikono, kukataa moja boma.
Hawajui pigo nono, laja wana pokoroma.
Ukimwi hauna dawa, tiba wala kafaara.

Kahaba nao husema, haba hujaza kibaba.
Hata hivyo wanazama, kwa hukumu yake Baba.
Ijapokuwa natama, wana maradhi si haba.
Ukimwi hauna dawa, tiba wala kafaara.

Vijana nawasihini, tuwachane na madawa.
Nawaasa nyi jamani, hatutaupata wawa.
Tujitie vitabuni, tukatae kufanyiwa.
Ukimwi hauna dawa, tiba wala kafaara.

Nasi wale tuloachwa, twayahitaji mapenzi.
Iwe asubuhi au chwa, kuntu yasiwe ya tanzi.
Ili tuwe kama mchwa, pia tuwe na ulinzi.
Ukimwi hauna dawa, tiba wala kafaara.

Tuwafundishe yatima, tupate nazo baraka.
Tusivirekodi vima, nao watatajirika.
Hawatapata nadama, na hawatatamauka.
Ukimwi hauna dawa, tiba wala kafaara.

Tamati sasa nafika, nami natia nanga.
Natumai mewapachika, mawazo yakumpanga.
Yasije sahaulika, kwani yashinda upanga.
Ukimwi hauna dawa, tiba wala kafaara.
PAUL KING’ORI,CHUO KIKUU CHA MOI.

2 comments: