Thursday 22 March 2012

KURUNZI YA KANISA FM....1

Ifuatayo ni taarifa ya habari ya Kanisa FM moja kwa moja kutoka Biblical Avenue, Inspiration House. Lakini kwanza tupate vimulimuli;
VIMULIMULI:
Ziwa Lawa nchi kavu…
Vijana ni muhimu…
Timu ya Ayubu ya shinda nishani ya dhahabu… Na
Nyote mwaonywa.
Hujambo na karibu mimi ni msimulizi wako Paul King’ori.
Na habari timilifu ndio hii.
  Huku vitendo vya Ilahi vikizidi kunoga na kumakisha mno, hapo jana aliendelea kuwastajaabisha wazalendo  Waisraeli. Wana hao waliokuwa wamekosa imani na Mungu wao na pia kiongozi wao Mteule Musa, waligutuka kuona miujiza ya Mola. Mbele yao mlikuwa na ziwa jekundu na nyuma yao mlikuwa na jeshi la askari wa Firauni, chambilecho ukistaajabu ya Musa utayaona ya Firauni. Mola mwenye huruma tele aliligawa ziwa hilo mara mbili na wanawaisraeli wakapitia katikati kulikokuwa kumekauka kiasi cha kutoa vumbi. La kuhangaisha ni kuwa, Waisraeli walipopita wote ng’ambo ya pili, ziwa lilirudi pahala pake na wanajeshi wa Firauni wakazama fyu! Usisahau kuwa Waisraeli walikuwa salama salimini.
 Waziri wa mashauri ya vijana Profesa Kohelethu leo asubuhi, alitoa hotuba kutoka kitabu chake Mlango wa 2:13-14. Akizungumza na Kanisa FM alitueleza kuwa, vijana wanafaa kuwa na macho pajini mwa nyuso zao ili waweze kuona mbele na mbali, sio tu kwa maisha bali kwa maisha ya kiroho hususani ya kibinafsi.
   Kikundi kisicho cha serikali yaani (NGO) kinachotetea haki za vijana kimetoa habari ya kuwaasa vijana haswa wakati huu tunakaribia mwisho wa mwaka kwa hivyo sherehe mbalimbali. Kwa mujibu wa ripoti zilizotumwa katika vyumba vya habari, zilisema kuwa mwenyekiti wa kikundi hicho anayeitwa Mteule Suleimani, alisema kuwa maji ya kuibiwa huwa matamu na mkate wa sirini hupendeza, hivyo basi wajikinge na anasa zisizofaa. Pia alinukuliwa akisema kuwa njia za wavivu hujaa miiba lakini njia za watu wenye bidii huwa kama barabara nyororo. Kwa hii alimaanisha kuwa wajihusishe na mambo yatakayotoa ufanisi maishani. Hii ni ripoti iliyotoka kitabu cha Methali 9:17 na Methali 15:19.
HABARI ZAIDI
  Ni dhahiri shahiri kuwa Kanisa FM ipo ili kukujulisha mambo yanapoibuka kila kuchao. Habari zinazonifikia sasa hivi zinasema kuwa Bwana Yesu mwana wa pekee wa Mungu anatarajiwa kutua ulimwenguni hivi karibuni. Duru za kuaminika zimetuarifu kuwa kulingana na Yohana, Binguni ipo na pia kuna Ahera. Hii ni ripoti kutoka Ufunuo 22:20
KURUNZI MICHEZONI
  Klabu bingwa mtetezi wa kanisa cha Ufanisi kinachoongozwa na kinara hodari Mungu Mtakatifu leo asubuhi kiliichapa timu ya kocha mlalahoi shetani bao 7-0. Bao zote zilipeperushwa wavuni na mchezaji hodari na wakujitolea muhanga Ayubu aliyesaidiwa na Roho Mtakatifu. Bao hizo zilikuwa za ushindi mkumbwa maanake ziliiwezesha timu ya Ufanisi Football Club kuchukua nishani ya dhahabu. Ayubu alirudishiwa mali yake maradufu. Mchezo huo uliokuwa na wasiwasi baada ya kocha duni shetani kujaribu kumhonga refa kwa kumwambia Ayubu amlaani Mungu, kitendo ambacho kilimfanya shetani apewe kadi nyekundu yaani ‘Red Card’.
HALI YA ANGA
Leo jioni kutakuwa na utulivu wa mapenzi ya Mungu, Mwana na Roho Mtakatifu.
Hatimaye kutakuwa na joto jingi kutokana na neno litakalotolewa na mhubiri leo hii.
Naam kadi ya tamati nimefika. Nakutakia wakati murua mimi ni Paul King’ori.
Kumbuka kuwa: Tunaweza kufanya mambo yote kutokana na mwenye kutupa nguvu.

1 comment:

  1. Top 5 Asian Betting Sites in 2021 - LegitBet.co.kr
    1XBet, known for its innovative, mobile-friendly, sports 바카라 betting app, is 1xbet korean licensed in South Korea and is part of the SBC Group of febcasino operators. 2

    ReplyDelete